Habari
TANZANIA NI MIONGONI MWA NCHI ZINAZOLINDA NA KURITHISHA UTAMADUNI WAKE
Tanzania imeendelea kuwa miongoni mwa nchi Duniani zinazoheshimu tamaduni za jamii yake pamoja na kuhifadhi, kuendeleza na kurithisha kwa vizazi vya sasa na baadae.
Hayo yameelezwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Methusela Ntonda, wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Uanuai wa Utamaduni yaliyofanyika Mei 21, 2026 Zanzibar.
Bw. Ntonda alieleza kuwa, Tanzania iliridhia Mkataba wa UNESCO wa mwaka 2005 wa kulinda na kuendeleza Uanuwai wa Kiutamaduni, ambapo amesema lengo la siku hiyo ni kutangaza na kujivunia utamaduni, kuhimiza uzalendo na amani.
Aidha, alisema katika kukuza na kueneza lugha ya kiswahili duniani Wizara ya Habari Utamaduni, Sanaa na Michezo kushirikiana na Wizara ya Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo ya Zanzibar, zimeandaa Kongamano la Kiswahili nchini Ufaransa katika Jiji la Paris litakalofanyika tarehe 4 - 7 Julai 2026.
Alitoa wito kwa Watanzania waliopo nchini humo, kuungana pamoja siku hiyo ili kutangaza utamaduni wa mswahili duniani.
